LIGI ya soka ya vijana wenye umri chini ya miaka 17, Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam, inatarajiwa kuanza leo kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari ya Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Chama cha Soka kwa Vijana Wadogo Wilaya ya Ilala (IDIYOSSA), Edwin Mloka ‘Father’, alisema kwamba maandalizi yamekamilika.
Alisema kwamba mchezo wa kwanza utafanyika saa 3:00 asubuhi, ambapo Manchester Kids itakipiga dhidi ya Msikate Tamaa, wakati mechi ya pili itawakutanisha Liwiti Kids dhidi ya Mdawa.
Mloka alisema kuwa mgeni rasmi katika michuano hiyo leo anatarajiwa kuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Soka Wilaya ya Ilala (IDFA), Mohammed Binda.
Mshindi wa kwanza katika michuano hiyo atazawadiwa seti moja ya jezi pamoja na sh 100,000 wakati mshindi wa pili atapata mipira miwili na mshindi wa tatu atapata mpira mmoja.
Timu nyingine zitakazoshiriki ligi hiyo ni Simba Kids, Dar Newala, Zalagoza, Mwiba Kids, Survivor Kids, Mogo Kids, River Heroes na DG Professionals.