MMOJA wa wanyama aina ya faru weusi ambao ni adimu na wanaothaminika zaidi duniani, ameonekana ndani ya eneo lililo chini ya uongozi wa kampuni ya kitalii ya Grumeti Reserves Limited katika Wilaya ya Serengeti, mkoani Mara.
Habari za uhakika zilizopatikana jana wilayani hapa, zimesema mnyama huyo alianza kuonekana Ijumaa iliyopita katika eneo la Nyakitono linalopendekezwa kuwa Jumuiya ya Uhifadhi wa Wanyamapori (WMA) ambalo ni sehemu ya eneo linaloendeshwa na kampuni hiyo ya Kimarekani.
“Faru mweusi wa kike ambaye bado hajajulikana alikotoka, alionekana akichunga katika eneo la Nyakitono… hiyo ni neema kubwa kwetu, kwani wanyama wa aina hiyo ni adimu sana duniani,” alisema ofisa mmoja mwandamizi wa Kampuni ya Grumeti Reserves aliyetoa sharti la kutotajwa jina gazetini.
Kuonekana kwa mnyama huyo katika eneo hilo ni dalili nzuri za kuwahifadhi faru weusi 25 wanaotarajiwa kupelekwa siku chache zijazo ndani ya eneo linaloendeshwa na kampuni hiyo kwa kibali cha Serikali ya Tanzania.
Inaelezwa kuwa faru ni miongoni mwa wanyama ambao idadi yao imekuwa ikipungua kwa kasi kubwa duniani katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.