KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Tanzania, ‘Taifa Stars’, Mbrazil Marcio Maximo, amekunwa na kiwango cha wachezaji chipukizi wa timu hiyo na kusema, wamempa shauku ya kuwapima wengine zaidi.
Maximo aliyetwaa mikoba ya timu hiyo Agosti 8, mwaka huu kutoka kwa Mzalendo, Dk. Mshindo Msolla, aliyasema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita wakati akizungumzia mechi iliyopita dhidi ya Burkina Faso na ijayo dhidi ya Msumbiji.
Alisema, wachezaji kama Henry Joseph na Athumani Iddi wa Simba, na Nizzar Khalfan wa Mtibwa Sugar ya Morogoro kwamba, licha ya ugeni wao katika kikosi hicho, wameonyesha uwezo mkubwa.
Maximo alisema, uwezo wa wachezaji hao umedhihirisha kwamba, soka si majina makubwa, hivyo ataendelea kuwapika chipukizi wengine kulingana na kiwango chao na si majina.
Kuhusu wachezaji kadhaa wanaotajwa kuwa wanafaa kuwamo katika kikosi hicho, Maximo alisema hamchukui mchezaji Stars kwa umaarufu wake bali kiwango.
Alisema, ipo siku Stars itakuwa na kiwango cha hali ya juu huku ikiwa haina wachezaji wenye majina makubwa, ingawa alisema, ni muhimu kwa timu ya taifa kuwa na wachezaji wanaocheza nje ya nchi.
Maximo alisema Stars isitarajie mteremko katika kundi lake, kwani kadiri inavyofanya vizuri, ndivyo inavyozidi kujijengea mazingira magumu kutokana na wapinzani kukaza buti tofauti na awali.
Akitoa mfano hai, Maximo alisema baada ya kufungwa na Senegal na kusikia Stars imeishinda Burkina Faso, Msumbiji imeamua kuwaita wachezaji wake wa kimataifa kukabiliana na Stars katika mechi ijayo.