MIAKA mitano baada ya magaidi kusababisha maafa makubwa nchini hapa, raia wa Marekani na washirika wake jana walianza kuadhimisha kumbukumbu hiyo kwa kuendesha maombi kimya kimya na kuweka mashada ya maua jana na kuwaomboleza watu karibu 3,000 waliopoteza maisha Septemba 11, 2001.
Katika eneo ambalo palikuwa pamesimama jengo refu la Kituo cha Kimataifa cha Biashara (WTC), waombolezaji waliomba kimya kimya kwa nyakati nne tofauti za saa 2:46, 3:03, 3:59 na 4:29.
Saa hizo ndizo ambazo ndege mbili zilizogeuzwa kuwa mabomu zilipobamiza na kuangusha minara pacha ya jengo.
Wake kwa waume na washirika wa watu 2,749 waliokufa kwenye kituo hicho walikuwa wakisoma majina ya ndugu zao huku wakiweka mashada ya maua.
Rais George Bush alitembelea eneo hilo juzi na jana alitarajia kutembelea maeneo mengine yaliyoshambuliwa ya Shanksville, ambako watu 40 walikufa wakati ndege iliyokuwa ikiaminika kwenda kubamiza Ikulu ya Marekani ilipoanguka kabla ya kutimiza lengo na makao makuu ya Wizara ya Ulinzi, Pentagon ambako watu 184 waliuawa.
Bush pia alitarajia kutoa hotuba maalumu kwa maadhimisho hayo ofisini kwake jana.
Pia familia za wahanga zilitarajia kufanya maombi saa 8:46 kwenye kiwanja cha ndege cha kimataifa cha Logan huko Boston.
Ndege za Shirika la Ndege la American Airlines na Shirika la Ndege la United Airlines aina yenye namba 175 ziliruka kutoka Logan kabla ya kugeuzwa mabomu kwenye minara hiyo pacha.
Utawala wa Bush umeripotiwa ukijigamba kwamba baada ya mashambulizi hayo umefanikiwa kuzuia mashambulizi mengine ya kigaidi pamoja na kuwapo kwa mgawanyiko mkubwa nchini hapa juu ya uvamizi wa Iraq, mateso dhidi ya watuhumiwa ugaidi na mbinu za kuwahoji.
“Hakukuwa na mashambulizi mengine nchini Marekani. Na hilo halikuja hivi hivi, na si bahati, bali baada ya kazi ngumu ya kuziba mianya yote,” Makamu wa Rais, Dick Cheney aliiambia televisheni ya NBC.
AP