WAKAZI wa Kata ya Sepeko wilayani Monduli, wamechanga ng'ombe zaidi ya 200 ili kusaidia ujenzi wa shule ya sekondari katika kata hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya mkutano wa kuhamasisha mchango huo katika Kijiji cha Mti Mmoja juzi, diwani wa kata hiyo, Loota Sanare alisema ng'ombe hao wamechangwa na wananchi wa vijiji vinane vya kata hiyo.
Alisema hivi sasa bado michango inaendelea katika kata hiyo na lengo ni kukusanya sh zaidi ya milioni 400 ambazo zitaweza kukamilisha sekondari hiyo.
Sanare alisema kutokana na makubaliano waliyofikia, kila kijiji kimekubali kuchangia ujenzi wa madarasa mawili na nyumba za walimu na kulingana na uwezo, vijiji vingine vimekubali kujenga ofisi.
Alisema vijiji ambavyo vinachangia ujenzi huo ni pamoja na Alkaria, Alkatan, Repolko, Losimongori, Lashaine, Lendikinya, Meserani Juu na Mti Mmoja.
Diwani huyo alisema sekondari hiyo, inatarajiwa kujengwa katika Kijiji cha Mti Mmoja na itajulikana kama Nanja Sekondari na itaanza na wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne.