WANACHI wa mji wa Tunduma wilayani Mbozi, wataendelea kupata shida ya maji hadi hapo mpango wa vichocheo vya mafanikio haraka (Quick wins) utakapoanza kutekelezwa.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Maji, Stephen Wassira katika ziara yake ya kutembelea miji ya Tunduma na Mlowo wilayani Mbozi, ili kujionea uhalisi wa tatizo la upatikanaji wa maji na kuona ni jinsi gani serikali inaweza kuchukua hatua za uboreshaji huduma hiyo.
Alisema serikali imetenga sh milioni 20 ili kusaidia kupunguza makali ya tatizo la maji wakati mpango huo unaandaliwa.
Meneja wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka mjini hapa, Justin Munishi amemweleza waziri kuwa tatizo la maji limedumu kwa takribani miaka 40 na kwamba mamlaka yake imekosa uwezo wa kulitatua kutokana na uwezo kifedha.
“Tatizo la uhaba wa maji limetokana na ongezeko la watu ambao ni wahamiaji wanaohamia mjini hapa kwa ajili ya biashara na kwamba wanahitaji meta za ujazo 1,234 kwa siku, lakini miundombinu iliyopo ina uwezo wa kuzalisha meta za ujazo 355,” alisema.