SIKU chache baada ya Moro United kupigwa faini ya dola 5,000 za Marekani (zaidi ya sh 500,000) baada ya kugomea mechi ya Kombe la Tusker dhidi ya Yanga, timu hiyo imepigwa faini nyingine ya kiwango hicho cha fedha na Shirikisho la Soka la Afrika (CAF).
Hatua hiyo imetokana na utovu wa nidhamu wa wachezaji wa Moro United waliouonyesha katika mechi ya kuwania Kombe la Shirikisho hilo dhidi ya Etoile du Sahel, mchezo uliofanyika mjini Sousse, Tunisi.
Ofisa Uhusiano wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Florian Kaijage, alisema kwamba uamuzi huo ulitolewa na Bodi ya Nidhamu ya CAF iliyokutana Agosti 30, mwaka huu jijini Cairo, Misri.
Kaijage alisema kwamba bodi hiyo ilipitia taarifa ya mwamuzi wa mchezo huo iliyoonyesha kwamba wachezaji watano wa Moro United walionywa kwa kadi za njano, hivyo kwa mujibu wa kanuni ya nidhamu ya CAF ibara ya 122, idadi hiyo ni moja ya matukio yanayoonyesha utovu wa nidhamu na inastahili adhabu.
Alisema katika barua ya CAF, imeeleza kwamba fedha hizo ni lazima zilipwe kupitia TFF ndani ya siku 60 kuanzia tarehe ya kupata taarifa. Tayari Moro United wamearifiwa juu ya uamuzi huo wa CAF.
Hiyo itakuwa faini ya pili kwa timu hiyo katika kipindi cha wiki mbili, kwani wiki iliyopita TFF iliitoza faini kama hiyo, kufungiwa kucheza michuano ya Tusker kwa miaka miwili pamoja na kupokonywa magoli mawili baada ya kugomea mchezo dhidi ya Yanga.