MAKAMU wa Rais, Profesa Gilbert Bukenya, ameeleza jinsi alivyoweza kurudi nyumbani salama kutoka Bangkok, Thailand, ambako kulitokea mapinduzi ya kijeshi.
Bukenya aliyeonekana mchangamfu aliliambia Gazeti la Daily Monitor nyumbani kwake huko Kakiri, Ijumaa iliyopita kwamba alilindwa vyema wakati serikali ya nchi hiyo ilipoangushwa.
“Nililindwa kwa kikosi chenye magari ya Mercedes Benz yapatayo sita na walinzi 27 nikiwa kwenye hoteli niliyofikia,” Bukenya alisema.
“Baadhi yao walikuwa askari polisi, wengine walikuwa makachero wa upelelezi na wengine kutoka jeshini. Lakini nilivyosoma magazeti asubuhi hii (Ijumaa), watu walikuwa wakisema kwamba Bukenya amekwama kwenye chumba cha hoteli. Kivipi?” alihoji.
Wakati Daily Monitor lilipomtembelea Bukenya kwenye makazi yake, alivaa ukakamavu wa kijeshi na alikutwa akiwahutubia wakazi wa Busiro Kaskazini ambayo ni sehemu ya jimbo lake, juu ya mbinu mpya za kubuni njia za kujijengea utajiri kwa njia ya ulimaji wa mpunga, mahindi na maharage.
Wiki iliyopita, Bukenya alijikuta katika wakati mgumu muda mfupi baada ya mapinduzi wakati alipoalikwa kwa chakula cha usiku na aliyekuwa Naibu Waziri Mkuu Chidchai Vanasatidya, kwenye Ikulu ya nchi hiyo. Siku iliyofuata Ikulu iliangukia mikononi mwa wapangaji wa mapinduzi hayo waliofanikiwa kumuangusha Waziri Mkuu Thaksin Shinawatra, kutoka madarakani huku Vanasatidya akitiwa mbaroni.
Lakini wakati habari za mapinduzi zilipoibuka, Profesa Bukenya alikuwa akifurahia maisha, kwa mujibu wa katibu wake wa habari.
Pia alitembelea Taassisi ya Kilimo cha Mpunga ya Thailand na Kampuni ya Sor Heng Noodle.
“Wakati makamu wa rais alipofanikiwa kurudi hotelini kwake, hakukuwa na matatizo yoyote kwani alienda kufanya mazoezi ‘gym’. Na alikuwa akifurahia maisha hotelini kabla ya kuibuka kwa habari za mapinduzi,” Katibu huyo Linda Nabusayi, alisema katika taarifa yake juzi.
“Nyakati za asubuhi, hakukuwa na dalili za mapinduzi mitaani na shughuli za kila siku ziliendelea kama kawaida. Habari pekee tulizoletewa na wenyeji wetu zilisema: “Kutokana na matukio yaliyotokea usiku wa jana, tunashika madaraka ya shughuli za kiserikali na balozi zote zimeshauriwa kwa mwenendo mzima wa leo. Leo imetangazwa siku ya mapumziko kitaifa na shughuli zote za kibiashara, shule, mabenki na ofisi za serikali zimefungwa.”
Hata hivyo, Bukenya alisema kwamba alishtushwa na kuingiwa na hofu na habari za kuangushwa kwa wenyeji wake lakini alipata imani wakati mkuu wa usalama wake aliyemhakikishia kwamba hakuna haja ya kushtuka kwani kila kitu kipo mahali pake.
Pamoja na kuhakikishiwa usalama hata hivyo aliambiwa asitoke hotelini pamoja na kwamba alihakikishiwa kwamba programu yake ya kutembelea maeneo mbalimbali haitaingiliwa. Bukenya alisema kwamba alifanya mikutano na wafanyabiashara maarufu wa Thailand waliosema kwamba watakubaliana na serikali mpya.
MONITOR