KESI ya kupinga matokeo ya uchaguzi jimbo la Mwibara, inaendelea kusikilizwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Musoma chini ya Jaji Francis Mchome.
Jumatano wiki hii, mashahidi ambao ni aliyekuwa Ofisa na Injinia wa Idara ya Maji wa Wilaya ya Bunda, pamoja na Ofisa Idara Utumishi ambaye pia alikuwa ni msimamizi msaidizi wa Tume ya Uchaguzi Mkuu katika Jimbo la Mwibara wilayani humo, walitoa ushahidi wao.
Kwa upande wake, Christopher Nyandiga, alitajwa na upande wa mlalamikaji, Mtamwega Mugaywa, ambaye alikuwa mgombea wa TLP, kuwa alishiriki katika kampeni.
Mugaywa alidai kuwa akiwa Ofisa wa Maji wa serikali, Nyandiga alisaidia pia kuchimba visima vya maji ili kumpa ushindi mgombea wa CCM, Charles Kajege, kitu ambacho Nyandiga alikikanusha katika ushahidi wake.
Shahidi huyo aliieleza mahakama kuwa mpango wa kuchimba visima hivyo ulikuwa katika mpango maalum ulioanza Julai hadi Desemba 2005, na katika utekelezaji huo kulikuwa na mashirika matatu ambayo yangehusika katika uchimbaji wa visima hivyo katika vijiji sita.
Nyandiga, ambaye alitajwa mara nyingi na upande wa mlalamikaji, alisema pamoaj na miradi hiyo, ilikuwepo pia miradi mingine ambayo ilikuwa chini ya vijiji moja kwa moja chini ya mradi wa mazingira (LIVEMP) pamoja na VIP.
Aidha, alikanusha vikali kutumika kwa gari la serikali lenye namba za usajili STJ 8094, kumfanyia kampeni mgombea wa CCM na hata kushiriki katika kampeni za uchaguzi mkuu kwa madai kuwa yeye alikuwa mtumishi wa serikali na wakati huo alikuwa na likizo akimuuguza mama yake mzazi katika hospitali ya rufaa ya Bugando jijini Mwanza.
Naye Kabubi Mbondo ambaye alikuwa Ofisa wa Utumishi Wilaya ya Bunda na Mkurugenzi Msaidizi wa Uchaguzi, akitoa utetezi wake, alisema kuwa mgombea Stella Julius hakuwa mgombea wa CCM Viti Maalum, ila alikuwa ni mgombea kupitia TLP.
Ili kuthibitisha hilo, alitoa barua yenye kumbukumbu namba TLP/UCH/VM/VOL1/01/2005, iliyomtambulisha na mgombea huyo alichukua fomu Septemba 9, 2005 kwa tiketi ya TLP.
Aliieleza mahakama hiyo kuwa Halmashauri ya Bunda hutoa magari baada ya kuombwa na watendaji ili kusaidia kubeba vifaa vya ujenzi katika miradi ya maendeleo bila malipo na alifanya hivyo kwa gari lenye namba za usajili SM 1305 kwa kutumia utaratibu uliopo kwenye halmashauri hiyo wa TMIS.
Alisema alitoa gari hilo kwa stakabadhi namba 0596 iliyotolewa tarehe 6 hadi 8 mwaka 2005 ili gari hilo litumke katika shughuli iliyopangiwa na mtendaji wa Kata ya Mwitende.