SERIKALI inadaiwa jumla ya sh 2, 111,173,148 na watumishi wa sekta ya afya nchini, ikiwa ni madeni ya likizo, kazi za ziada, uhamisho, gharama za masomo na matibabu.
Kati ya deni hilo, Mkoa wa Singida unadai sh 95,745,319 kwa ajili ya watumishi 529 waliopo kwenye maeneo mbalimbali mkoani humo.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Celina Kombani, alisema watumishi wa Hospitali ya Mkoa wa Singida wanadai sh 34,180,900 wakati Halmashauri ya Wilaya ya Singida inadai sh 32,472,302, huku Halmashauri ya Wilaya ya Iramba ikiwa inadai sh 20,501,117, Manispaa ya Singida (sh 4,478,000) na Wilaya ya Manyoni sh 3,113,000.
Akijibu swali lililoulizwa na Mbunge wa Viti Maalum, Diana Chilolo (CCM), Kombani alisema katika kipindi cha Februari 2007, serikali ilifanya uhakiki wa madai mbalimbali ya walimu na tayari madai yaliyobainika yamewasilishwa Hazina kwa hatua za malipo.
Alibainisha kuwa mkakati wa serikali ni kuhakikisha kuwa madeni yake yote kwa watumishi wake yanalipwa na ili kutekeleza mkakati huo imeziagiza halmashauri zote nchini kutenga fedha katika bajeti zake kwa ajili ya kulipa madai ya watumishi ili kuepuka malimbikizo ya madeni.
Aidha, alisema kuwa serikali inatarajia kuhakiki madai ya watumishi wa Afya kama ilivyofanya kwa madeni ya walimu ili kuwaondolea kero ya malimbikizo watumishi wa Sekta ya Afya nchini kama ilivyo kwa walimu.
Alisema kuwa zipo halmashauri ambazo tayari zimekwishaanza kutekeleza agizo hilo zikiwamo halmashuri za mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Mtwara na Rukwa ambazo zimefanikiwa kulipa madeni yote ya watumishi wake.
Alizitaja pia halmashauri ambazo bado kabisa hazijaanza kutekeleza zoezi hilo na zinadaiwa na watumishi wake kuwa ni kutoka katika mikoa ya Pwani, Kilimanjaro, Mbeya, Morogoro, Mwanza, Shinyanga na Manyara.
Chilolo katika swali lake alitaka kujua kama serikali inazo takwimu za madeni ya watumishi wake kwa nchi nzima na Mkoa wa Singida, na mikakati iliyopo katika kuhakikisha kuwa madeni yote ya watumishi wa serikali yalipwa na mikoa ambayo haidaiwi madeni na watumishi wake.