WAZIRI wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, amesema baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Kigoma, yatapata umeme wa uhakika Desemba 2009.
Alisema kuchelewa kwa mpango wa serikali kufikisha umeme mkoani humo kunatokana na taratibu ndefu za uagizaji wa mashine mpya ya kuzalisha umeme kutoka nje.
Karamagi alilazimika kutoa ufafanuzi huo baada ya swali la nyongeza la Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba (CCM), aliyetaka kufahamu sababu za ahadi ya Rais Jakaya Kikwete ya kufikisha umeme katika mkoa huo kusogezwa.
“Nataka kufahamu…wakati Rais Kikwete alipotembelea Kigoma aliahidi kuwa tutapata umeme Januari 2009, leo naibu waziri anasema tutapata umeme huo Desemba 2009, kwa nini mnachelewa?
“Wakati wenzetu wanazungumzia kupeleka umeme vijijini sisi tunatarajia kuona umeme kwenye ofisi ya makao makuu ya mkoa...hivi ni lini Kigoma tutapata huduma hii kwa uhakika?” alihoji Serukamba kwa masikitiko.
Katika majibu yake, Karamagi alisema ili kuondoa upungufu wa umeme mkoani Kigoma, serikali imeagiza mashine mpya yenye uwezo wa kuzalisha kilowati 2,000 na kwamba makubaliano kati ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na Kampuni ya Anglo Belgium Corporation yamekamilika na unatarajia kuingia nchini Desemba 2009.
Katika swali la msingi, Serukamba alitaka kufahamishwa hatua zilizofikiwa za utekelezaji wa mpango wa kuupatia Mkoa wa Kigoma umeme wa uhakika na mkakati wa kuweka umeme wa dharura wakati ukisubiriwa muda wa utekelezaji wa mpango wa awali.
Aidha, Waziri Karamagi alibainisha kuwa katika kipindi cha mwaka 2008 hadi 2012, serikali itajenga kituo cha kuzalisha umeme wa maji kwenye Mto Malagarasi kitakachotoa kilowati 8,000. Mradi huo utafadhiliwa na Millenium Challenge Corporation (MCC) la Marekani.