NAJUA hamkawii kusema Mzee wa Kujitoa amechanganyikiwa. Semeni tu mkitaka lakini ni haki yangu ya kikatiba kusema na hata kuota ndoto. Tulikofikia natamani ningekuwa na madaraka nawaapia. Kwani dhambi kutamani madaraka? Mbona wapo wanaoyatafuta hata kwa kuhonga? Huko simo mototo wa mama lakini nasema ole wenu siku hiyyo nitakapobahatika kukalia odfisi kubwa zaidi hapa nchini.
Mwanangu nakuapia ningeanza kupambana na mafisadi. Mwadhani ningewaonea haya hao watu hata kama wana majina makubwa pengine na fedha nyingi? Hao mbona ndio wa kwanza kuanza kuwafuatilia nijue uhalali wa hizo njululu mwangu? Kwangu hakuna hakungekuwepo cha mwaswalie mtume nawaapi. Nyie nipeni tu kura muone!
Mwadhani watu wanaotuingiza mkenge kwa mikataba isiyo na kichwa wa la miguu wangesalimika? Nawaapia hao wangejieleza wakiwa lokapu ya maafande. Mbona vibaka wanaokwapua maandazi na vitumbua wanawekwa lupango? Mwizi si mwizi tu? Tena anayetuingiza mkenge mbona ndie anapaswa kutolewa kafara wa kwanza? Huko simo lakini nadhani tofauti yangu na hayati Edward Sokoine ingekuwa ndogo wandugu.
Eti mtu atuhumiwe kwa kuhujumu, kufuja au kuiba halafu atarajie kuendelea kubaki kwenye ofisi ya serikali akipulizwa na kiyoyozi? Hilo lisingetokea asilani! Jambo la kwanza ingekuwa kumshauri ajiuzulu mwenyewe kupisha uchunguzi huru akikataa ndipo nampiga ngwala aondoke ili tumchunguze vyema.
Nani aliwadanganya panya anaweza kujifanyia mambo yake vizuri wakati paka akiwa karibu? Mbona kuwaacha watuhumiwa ofisini halafu kudai unawachunguza ni sawa na kumwambia panya alale na paka? Kwangu hayo hayapo mwanakwetu.
Hamkawii kuniona ninayehukumu kwa jazba. La hasha. Hiyo si ni ofisi ya umma mwanakwetu? Ukituhumiwa tu si yatosha kukufanya uachie wengiene wasio na kashfa kutumikia ofisi hiyo? Kwani bila wewe taifa halipo mwanakwetu? Mmesahahu ile hadithi isemayo mke wa mfalme hata akisingiziwa kushiriki ufuska shuruti auachie umalkia? Kwenu hicho ni Kigiriki siyo? Mwenzenu huko simo, lazima nijitoe.
Hayo ya ubaka uchumi nawaapia ningeyakomalia kishenzi. Mbona hata kama ikibidi ningeamuru mirija yote inayotorosha utajiri ikatwe? Kwani si kazi rahisi tu? Unajiuliza rasilimali ipi inamnufaisha nani na kwa nini. Kama jibu rasilimali iko kwenye kaya halafu yamnufaisha mgeni si ndio unakuwa mbogo? Nawaapia hata diplomasia ingenishinda kwa minajili ya watu kufaidi chao. Hata Mugabe pamoja na mapungufu yaken mwadhani ni mjinga kuwaambia wtatoto wa malkia wawaachie Waafrika ardhi yao? Mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni.
Nisingeruhusu kuzungukwa na watendaji wanaozomewa wakienda kwa wananchi. Mbona kuzomewa maana yake ni umma kukukataa? Nasema huko simo lakini nina hakika kuzomewa kwa sababu ya utendaji ingekuwa tiketi ya kukurudisha kwenu ukashiriki katika kilimo badala ya kubaki kufanya urasimu ofisini. Simo huko mwanakwetu.
Mwanangu nawaambia ndiyo maana hamnipi madaraka maana sio ajabu mngeishia kusema kichaa kapewa rungu. Wanaotafuna mali ya umma kama mchwa mwadhani hao ningewahurumia? Eti ule vya umma kwa mkono wa kuume na ule wa kushoto halafu utarajie bado mambo yatakuwa shwari? Nasikia wengine wanasema huko sio kula, ni kubugia. Mwanangu simo katika hayo yote.
Mwadhani katika utawala wangu huo wa kufikirika ningeshindwa kupata kipaumbele? Mbona kila kitu kinaanzia kwenye elimu wandugu? Mbona haya yalishasemwa tangu enzi zile za Baba wa Taifa? Kale kamsemo ketu kasemacho elimu ni ufunguo wa maisha mwadhani ni mzaha siyo? Mbona kama mwatambua ni ufunguo wa maisha uwekezaji kwenye elimu unazua mashaka?
Utaachaje kuzua mashaka nkama tunasikia habari za walimu wanaoitwa vodafasta? Huko simo labda ni maneno ya vijiweni. Eti iwezekane kweli mwalimu wa kufunza wanafunzi wa sekondari anaandaliwa katika wiki nne? Mbona huo ni muda tu wa kuyafahamu mazingira ya chuo? Hivi wanachopata kwa mafunzo hayo yasiyofika miezi mitatu ni shahada, stahada au astashada? Mbona mwatuletea ya Musa kabala hatujaona ya Firauni? Nishawaambia kwamba huko miye wala simo kabisa mtoto wa mama miye!
Bila elimu mbona ni wazi maisha yamejifunga. mesahahu ufunguo kazi yake kufungua? Mtaota maendeleo bila kuwekeza kwenye elimu? Mbona mkishindwa kusomesha watoto wenu mnakaribisha wageni kututawala? Mwadhani wakina Magungo wa Museveri wangekuwa na elimu wangeuza nchi kwa bei ya shanga? Sasa nini kitatokea mnaposhindwa kuwasomesha wanenu?
Eti katika zama hizi mnapowakaribisha watoto wa nyayo na wale jirani zetu waliotawaliwa na nduli bado mwafanya elimu lakshari siyo? Kama sivyo haya ya kukopesha mbona ni kiama kwa maskini? Urasimu wa kujaza hizo fomu mwausikia au mwaujua mwanakwetu? Na maskini atakopa halafu alipe na nini? Nilishawaambia siku nyingi sana kwamba mie huko simo kamwe.
Kwani mwadhani hatujui maisha bora hayaletwi kwa kucheza hicho mnachokiita ‘pool’? Mmewawezeshaje hao vijana wetu wanaomaliza shule kufanya shughuli nyingine badala ya kucheza ‘pool’? Eti ninyi kama si Mwalimu kuwapa opotuniti mwadhani mzingekuwa mnaendelea kucheza rede huko mtaani? Mwabisha kwamba ni wajibu wa watawala kuwatengezea watu wake fursa? Bila miundombinu mwadhani fursa zilizopo zaweza kutumika? Na hii elimu ya nadharia nayo bado mwaiona mali sana ? Nikae kimya katika hili.
Huko kwenye afya ngoja ninyamaze tu. Lakini niwadokeze tu katika utawala wangu wa kufikirika nisingetaka kusikia kitu kinaitwa ‘mashangingi’ ya viongozi wakati eti kuna watu waliojifungua wamelazwa mzungu wa nne! Dunia hii iliyojaa maambukizi mwathubutu hayo? Mbona hata yale magari tunayoyaita forokobe ni usafiri mzuri tu? Kuna raha gani kukaa katika gari la kifahari wakati wodi za waginjwa hazina vyandarua? Hamjisikii vibaya kusikia mgonjwa aliyekwenda kutibiwa tumbo anarudi akiwa na malaria? Nishasema huko simo maana hamkawii kuniita mchochezi mtoto wa mama mie.
kevinmakyao@hotmail.com
0784 265072