MWANAFUNZI mmoja, Aisha Ally (13), wa darasa la nne katika Shule ya Msingi Mlowa, iliyoko Tarafa ya Itigi, wilayani Manyoni, amefariki dunia katika jaribio la kutoa mimba.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Singida, Celina Kaluba, mwanafunzi huyo alifariki dunia muda mfupi baada ya jaribio la kumtoa mimba lililofanywa na mganga wa kienyeji, aliyefahamika kwa jina la Maria Isack (46), mkazi wa Kijiji cha Mlowa, Tarafa ya Itigi, wilayani Manyoni, kushindwa.
Kamanda Kabula alisema Aisha alikufa muda mfupi baada ya kufikishwa katika Hospitali ya Mtakatifu Gasper, Novemba nne, majira ya saa 11 jioni.
Alisema siku ya tukio, Aisha alikwenda kwa mganga wa kienyeji kwa dhumuni la kutoa mimba ya miezi minne. Kwamba mganga huyo alianza kumpa dawa za kienyeji za kunywa ili mimba itoke, kisha alimwamru alale chali, akachukua ‘spoku ya baiskeli’ na kuanza kumchoma nayo sehemu za siri.
Kamanda Kabula alisema muda mfupi baadaye, hali ya mwanafunzi huyo ilibadilika na kuwa mbaya, akalazimika kupelekwa hospitali ambako alifariki muda mfupi baadaye.
“Tumemkamata huyo mganga, tulipomfanyia upekuzi nyumbani kwake, tulimkuta akimiliki chupa mbili za dawa ya usingizi, mabomba ya sindano, gloves, pamba, bandeji na leseni ya uganga wa kienyeji,” alisema Kaluba.
Alisema polisi walifanikiwa kumkamata mganga huyo baada ya kupewa taarifa na mama mzazi wa Aisha kuwa alifariki wakati akitolewa mimba na mganga wa kienyeji na anatarajiwa kufikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.