WAKAZI wawili wa mjini hapa wameshitakiwa mahakamani kwa kosa la kutupa porini maiti ya mtu aliyekufa akiwa nyumbani kwa mganga wa kienyeji.
Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Inspekta Said Gingo, alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya, Juma Hassan kuwa washitakiwa walitenda kosa hilo Oktoba, 29 katika Kijiji cha Bunegezi, Bukombe mkoani Shinyanga.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mathias Hengeli (50) na Punja gwanzila (17), wote wakazi wa Kijiji cha Bunegezi, Shinyanga ambao walikuwa wakiishi nyumbani kwa mganga huyo kama wasaidizi wake.
Gingo aliendelea kueleza mahakamani kuwa washitakiwa walimtupa marehemu, Kasamwa Shilagila, aliyekuwa akitibiwa nyumbani kwa mganga huyo baada kufariki.
Alidai kuwa mganga huyo alitoroka baada ya kuona mgonjwa wake kafariki na wasaidizi wake waliamua kuuchukua mwili wa marehemu kwenda kuutupa porini ili kuondoa usumbufu wa kuulizwa na ndugu zake waliokuwa wakifika kumjulia hali nyumbani kwa mganga huyo.
Gingo alidai kuwa mwili wa marehemu uliokotwa na wasamaria wema ukiwa umeharibika lakini ndugu zake walifanikiwa kuutambua.
Washitakiwa walikamatwa baada ya kugundulika kuwa wasaidizi wa mganga na kupatikana taarifa za awali kuwa ndio walioubeba mwili huo kwenda kuutupa porini.
Washitakiwa walirudishwa rumande hadi Novemba 20 kesi yao itakapotajwa tena, na polisi wanaendelea kumsaka mganga wa jadi aliyekimbia.