TIMU ya netiboli ya Jeshi Stars ya Tanzania, jana ilifanikiwa kuivua ubingwa NIC ya Uganda kwa kuitwanga mabao 26-23 katika mechi ya michuano ya Kombe la Nje ‘Nje Cup’ iliyopigwa kwenye Uwanja wa TCC Chang’ombe, jijini Dar es Salaam.
NIC iliyokuwa ikiwania taji hilo kwa mara ya tatu mfululizo, jana ilijikuta ikizidiwa mbinu na wadada wa Jeshi Stars, ambako hadi ngwe ya kwanza inakamilika, ilikuwa imechapwa mabao 13-12.
Mechi iliyo iliyochezeshwa na Millicent Busoro na Asmaahoney Said na kushuhudiwa na mashabiki lukuki, ilikuwa ni ya ushindani mkubwa kwa muda wote.
Katika ngwe ya lala salama, NIC ilizidisha mashambulizi zaidi ili kutetea taji hilo, lakini maafande wa Jeshi nao walikuwa imara kuhakikisha wanawavua ubingwa.
Ndani ya dakika 10 za kipindi cha pili, NIC ikiongozwa na nahodha wao Betty Namukasa, waligoma kuendelea na mechi hiyo kwa madai waamuzi walikuwa wakipendelea wapinzani wao.
Betty alidai, mfungaji mahiri wa timu pinzani, Grace Daudi ‘Sister’ alikuwa akimlalia mlinzi wao ili afunge kirahisi bila waamuzi kuchukua hatua.
Hadi waamuzi hao wanamaliza mechi hiyo, Jeshi Stars walikuwa mbele kwa mabao 26-23, hivyo kufikisha pointi 12 na kutwaa ubingwa.
Walioing’arisha Jeshi ni Grace Daudi na Rebeca Masatu na kwa upande wa NIC, ni Amongin Florence na Namukaaga Babra.
Mshindi wa pili wa michuano hiyo ni JKT Mbweni waliomaliza wakiwa na pointi 11, huku NIC ikimaliza ya tatu kwa pointi 10.
Mchezaji bora wa kati wa michuano hiyo, ni Faraja Malaki wa CMTU, mzuiaji bora ni Monica Aloys wa JKU na mfungaji bora ni Grace Daudi ‘Sister’.
Mchezaji bora wa jumla wa mashindano hayo yaliyoanza Novemba 3 na kushirikisha jumla ya timu nane, ni Harriet Apako (NIC). Wote walipatiwa zawadi.
Aidha, kulikuwa na mchezaji bora kwa kila timu, ambako kwa CMTU ni Agnes Simkonda (GA), Halid Abdallah (GK) wa Chipukizi, Shinuna Mohammed (C) wa Afya, Magoli Khamis wa JKU, Betty Namukasa (NIC), Nelly Anyingisye (JKT) na Mpala Idd wa Jeshi Stars.
Mashindano yalifungwa rasmi na Kaimu Katimu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimatafa, Balozi Joram Biswaro, aliyezitaka timu ambazo hazikung’ara vema, kutokatishwa tamaa badala yake kujipanga upya.
Aliipongeza Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwa kuandaa michuano hiyo inayochangia kukuza ushirikiano na kushauri yawe yanashirikisha nchi za Afrika Mashariki na Kati ili kuimarisha uhusiano kupitia michezo.