CHUO cha VETA Mikumi, kimeahidi kuzalisha ajira zenye ushindani katika soko la ajira Afrika Mashariki na Kati zaidi ya robo ya ajira 1,000,000 zinazokusudiwa kutolewa na serikali ya awamu ya nne ifikapo mwaka 2010.
Sambamba na ahadi hiyo, chuo hicho kimeihakikishia serikali kuwa, katika mfumo mahiri wa ufundishaji (CBET), kitazalisha wahitimu watakaoshinda soko huria la ajira Afrika Mashariki na Kati, huku wengine wakijiajiri bila kutatizwa na kukua kwa teknolojia na utandawazi.
Kaimu Mkurugenzi wa VETA Makao Makuu, Alois Shayo, alimweleza hayo Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ludovick Mwananzila, aliyekwenda kutunuku vyeti kwa wahitimu 162 wa fani mbalimbali ikiwemo ya uongozaji watalii iliyoanza kutolewa hivi karibuni chuoni hapo.
“Mfumo wa CBET sambamba na utoaji vifaa vya kuanzia kazi kwa wahitimu unaotumiwa sasa na vyuo vya VETA nchini, unavifanya vyuo hivyo kuzalisha ajira badala ya wahitimu kama ilivyokuwa hapo awali,” alisema Shayo.
Awali, mkuu wa chuo hicho, Ramadhani Mataka, alimweleza Naibu Waziri huyo kuwa chuo hicho kinachoendesha mafunzo mbalimbali kwa muda mrefu na mfupi, tayari kimezalisha wahitimu zaidi ya 5,000 kati ya mwaka 2002 hadi 2007.
“Pia chuo kinafanya mazungumzo na vyuo vya juu hapa nchini, mfano Chuo cha Wanyama pori Mweka ili viwatambue na kuwaendeleza wahitimu wetu katika kiwango cha juu cha elimu kitakachowezesha kuwatoa wageni wanaokuja kutafuta ajira nchini mwetu,” alisema Mataka.
Alisema katika ajira hizo zinazotarajiwa kuzalishwa na chuo hicho kila mwaka, VETA Mikumi inakusudia kutoa wahitimu bora 1,700 wa fani ya uongozi wa watalii kwa mwaka ifikapo 2011.