RAIS Jakaya Kikwete, amemteua Magesa Stanslaus Kababi Mulongo kuwa Mkuu wa Wilaya ya Bukombe na kuwahamisha vituo vya kazi wakuu wa wilaya watatu.
Mulongo (37) anajaza nafasi iliyoachwa wazi na Hajat Amina Mrisho Said aliyeteuliwa hivi karibuni kuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa.
Waliobadilishwa vituo ni Albert Amiri Mnali, anayetoka Tunduru kwenda Bukoba; Paul Victor Chiwile anayetoka Bukombe kwenda Ukerewe na Peter Toima Kiroya, anayetoka Ukerewe kwenda Tunduru.
Mulongo ana shahada ya Biashara na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kabla ya uteuzi huu, alikuwa Meneja wa Kituo cha Biashara cha Mkoa wa Rukwa cha Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL).
Pia aliwahi kuwa mwalimu kwa muda katika Shule ya Sekondari Kibara na kufanya kazi kampuni ya simu ya Mobitel na kampuni ya vifaa vya ofisi ya Business Machine Ltd.