SERIKALI imekiri kushuka kwa kiwango cha kufaulu katika shule za sekondari kwa mwaka 2007 ikilinganishwa na matokeo ya mwaka 2006.
Hayo yalibainishwa bungeni mjini hapa jana na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mwantumu Mahiza, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Susan Lyimo (CHADEMA), aliyetaka kujua sababu za kuwepo kwa matokeo mabaya katika mwaka huo.
Akijibu swali hilo, Mahiza alisema kuwa hali hiyo ilijitokeza katika shule zote zikiwemo za seminari na shule za
serikali, ambapo katika wanafunzi waliofanya vizuri, 12 bora walitoka shule za serikali.
Hata hivyo, Mahiza alisema kuwa hadi hivi sasa, Serikali bado inaendelea kufanya tathmini kubaini sababu za
kushuka kwa kiwango hicho na maeneo yaliyofanya vibaya zaidi.
Alibainisha kuwa baada ya serikali kubaini sababu hizo, itachukua hatua za kuondoa kasoro hizo, ikiwamo kuboresha ufundishaji kwa kuwapeleka walimu katika mafunzo kwa masomo ambayo hayakufanywa vizuri.
Aidha, aliwataka wabunge kutowakatisha wananchi tamaa kuhusu shule za Sekondari za Kata badala yake wawatie moyo na kuwahimiza kuwa bajeti ya mwaka huu itaziwezesha shule hizo kufanya vizuri kwa kuongezewa walimu.
Alisema ili kuinua ubora katika kufaulu katika shule za sekondari za serikali, wizara yake imechukua hatua ikiwa ni pamoja na kuboresha ufundishaji kwa kuwapeleka katika mafunzo walimu wa masomo ambayo wanafunzi wamekuwa hawafanyi vizuri.
Aidha, alisema wizara inaboresha mazingira ya kufundishia, kujifunzia, ikiwa ni pamoja na kuongeza vifaa, kuajiri walimu zaidi, kujenga maabara, maktaba, nyumba za walimu katika shule za sekondari kulingana na uwezo wa kifedha.