WAANDISHI wa habari, Mariam Nkya, mwanafunzi wa mwaka wa kwanza katika Chuo cha Uandishi wa Habari, Dar es Salaam School of Journalism (DSJ), na Safina Kassanga wa Kampuni ya Mwananchi Communications, juzi usiku waling’ara katika kinyang’anyiro cha Miss Ukonga 2007.
Wanahabari hao waliwapeleka puta washiriki wengine, na Nkya kutawazwa kuwa malkia mpya wa kitongoji hicho, huku Kassanga akitwaa nafasi ya tatu, katika shindano lililofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita katika Ukumbi wa Free Time Resort, uliopo Ukonga jijini Dar es Salaam.
Katika mtanange huo, nafasi ya pili ilikwenda kwa Emmy Mtangi, wakati nafasi ya nne ilichukuliwa na mrembo Winfrida Joseph, nafasi ya tano ilishikwa na Hellen Lyimo.
Zawadi zilizotolewa katika shindano hilo ni pamoja na sh 200,000, kompyuta, nafasi ya kusoma kozi ya kompyuta pamoja na kufanya kazi katika idara ya matangazo na biashara katika Kampuni ya Uhuru Publications kwa mshindi wa kwanza.
Mshindi wa pili alipata sh 150,000, pamoja na seti moja ya luninga, huku mshindi wa tatu hadi wa tano walipewa kiasi cha sh 100,000 kila mmoja, wakati washiriki waliobaki walipewa kifuta jasho cha sh 40,000 kila mmoja.
Asia Idarous, ambaye ni mbunifu wa mitindo na mavazi, na mmiliki wa Kampuni ya Febark Fashion, ametoa zawadi ya kuwashonea mavazi watakayotumia warembo hao, katika kinyang'anyiro cha Miss Ilala, baadaye mwaka huu.