KITUO cha British Council, leo kinatarajiwa kutoa maelezo jinsi wasanii wa Tanzania watakavyoweza kushiriki katika mpango wa kuwasaidia utakaofanyika nchini Uingereza hivi karibuni.
Mpango huo unaojulikana kama ‘Bring Noise’, una lengo la kuboresha vipaji vya wanamuziki na wasanii kutoka nchi za Mashariki na Magharibi mwa Afrika.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kitengo cha mawasiliano cha British Council jana jijini Dar es Salaam, programu hiyo itafanyika kwa wiki mbili na itawasaidia katika kuendeleza vipaji vyao kwa kuwajengea uzoefu ndani na nje ya nchi zao.
Pamoja na mambo mbalimbali, wasanii hao wakiwa Uingereza, watapata
fursa ya kutengeneza nyimbo za pamoja zitakazowasaidia kubadilishana uzoefu jambo litakalowapa maendeleo wao wenyewe.
Pia taarifa hiyo ilisema kuwa, Bring Noise itasaidia kuendeleza mahusiano mazuri kati ya nchi za Mashariki, Magharibi mwa Afrika na Uingereza.
Nchi zinazotarajiwa kushiriki mpango huo ni Tanzania, Ethiopia, Kenya, Uganda, Ghana, Cameroon, Sudan, Nigeria, Siera Leone, Senegal na wenyeji Uingereza.