VYUO vikuu nchini vimetakiwa koboresha mitaala ya elimu kwa wanafunzi wa elimu ya juu, ili kuwawezesha wanafunzi kuingia kwenye soko la ajira.
Hayo yalielezwa mwishoni mwa wiki na Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), Dk. Batrida Burian, kwa niaba ya Waziri Mkuu, wakati wa mahafali ya kwanza ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT).
Burian alisema nchi zilizoendelea zimewekeza kwenye elimu na kupata wasomi wengi na kufungua milango ya uchumi wa nchi.
“Ninaamini taaluma mliyoipata mtaitumia vizuri katika maendeleo yenu wenyewe na taifa kwa ujumla, kwa kuonyesha ubora wa taaluma ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam,” alisema Waziri Burian.
Alisema Tanzania inatakiwa kuwekeza kwenye elimu zaidi kuweza kutambulika kwa kuwa na wataalamu wengi.
Aidha, aliwasihi wahitimu kutokuwa chanzo cha maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU).
Naye Waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter Msolla, alisema kwa sasa Tanzania haina wataalamu wa madini, lakini jitihada zinaendelea kuazisha kitengo hicho, ili kuweza kuwapata wataalamu hapa hapa nchini.