MBUNGE wa Tarime, Chacha Wangwe (CHADEMA), amelaani kitendo cha serikali mkoani Mara kuzuia mapokezi yake baada ya kuchaguliwa kushika nafasi ya makamu mwenyekiti wa chama hicho taifa, pamoja na kufanya mkutano wa kibunge na wananchi wa jimbo lake.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Moshi hivi karibuni akiwa na Kamati ya Bunge ya Kilimo na Ardhi, Wangwe alisema kitendo hicho ambacho kilileta vurugu ambazo zilisababisha polisi kuwajeruhi wananchi, hakijawahi kutokea nchini na kuongeza kuwa tukio hilo halistahili kufumbiwa macho, kwani linakwenda kinyume cha taratibu zilizowekwa kwa mbunge yeyote.
“Hili suala nitalihoji bungeni na zaidi tutakwenda mahakamani ili waliofanya vitendo hivyo wachukuliwe hatua za kisheria,” alisema Wangwe.
Alisema yeye kama mbunge ameweka utaratibu wa kukutana na wananchi wa jimbo lake kabla ya kwenda katika kikao cha Bunge kwa lengo la kufahamu matatizo yanayowakabili ambayo huyapeleka kama mapendekezo katika Bunge.
Wangwe alisema kutokana na kitendo hicho anakwenda bungeni bila kujua matatizo yanayowakabili wanacnchi wake, ikiwa ni pamoja na kupewa ridhaa na wazee wa Jimbo la Tarime.
Katika tukio jingine, Wangwe ameendelea kuulalamikia uongozi wa Mkoa wa Mara kwa kutaka kubatilisha maamuzi ya Baraza la Madiwani wa Wilaya ya Tarime ya kuwalipia wanafunzi wa sekondari wanaotoka katika wilaya hiyo.
Alisema kutokana na wananchi wa Wilaya ya Tarime kuwa nyuma kielimu kutokana na hali ya kiutamaduni, baraza la madiwani lilipendekeza kuwalipia wanafunzi 5,000 kuanzia mwezi huu.
Wangwe alisema kuwa alitegemea uongozi wa mkoa ungepongeza kitendo hicho, badala yake unakuwa mstari wa mbele katika kutaka kubatilisha maamuzi ya baraza la madiwani, na kuutaka uongozi wa mkoa kutoa kipaumbele katika masuala ya maendeleo na si kuangali masuala ya siasa.