WAKAZI wa Kata ya Visiga, wilayani Kibaha, Pwani wamelaani kitendo cha wanafunzi wa sekondari ya kata hiyo, kufukuzwa shule kwa kushindwa kuchangia madawati.
Wanafunzi hao wamefukuzwa kutokana na kushindwa kuchangia sh 80,000 kwa dawati moja.
Wakizungumzia suala hilo, wazazi hao walisema siku hizi walimu wamekuwa chanzo kikubwa cha kukwamisha wanafunzi kuendelea na masomo kwa michango mingine ambayo hata serikali haiitambui.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa niaba ya wazazi wengine, Tatu Juma alisema watoto wao ambao wamechaguliwa hivi karibuni kujiunga na kidato cha kwanza katika shule hiyo wameshindwa kuendelea na masomo kutokana na kukosa fedha ya kulipia madawati.
“Kwakweli tunashindwa kuwaelewa walimu wana malengo gani, kwani hata kama kuna fedha nyingine wanazifidia lakini hizi zimezidi, kwani sijawahi kusikia dawati moja likigharamiwa kwa sh 80,000 na walimu wakiambiwa wavumilie watoto waendelee kusoma, ili fedha hiyo itafutwe hawataki wanasema wasubiri mpaka fedha itakapopatikana ndipo waende kuendelea na masomo,” alisema Tatu.
Alisema ingawa serikali inawalaumu wakazi wa Mkoa wa Pwani kwa kuwa nyuma kimaendeleo kutokana na wengi wao kutowapeleka watoto shuleni, lakini kwa suala hilo liangaliwe upya ili wajue kwamba walimu pia wamekuwa chanzo cha kukwamisha maendeleo ya wakazi wa wilaya hiyo kwa kubuni mbinu za kupata fedha.
Alisema baadhi ya wazazi walijaribu kufuatilia Idara ya Elimu na kugundua kuwa hakuna michango kama hiyo, kwani wakati mwingine wanalazimishwa watoto wao wanunue sare zinazoshonewa shuleni, wakati zinauzwa kwa bei kubwa.
Naye Ally Kinyogoli, mkazi wa kata hiyo, alisema watoto wake wanaosoma shule hiyo wamefukuzwa kwa vile ameshindwa kulipa sh 160,000 kwa ajili ya kuchangia madawati mawili na kuiomba serikali iingilie kati suala hilo.
Alisema serikali kwa kuhakikisha kila mwanafunzi anapata elimu iliamua kufuta ada kwenye shule zote za msingi na kwa upande wa sekondari iliamua kupunguza ada hadi sh 20,000 ili kila mzazi aimudu, lakini walimu wanaamua kubuni michango mingine ambayo inasababisha kurudisha nyuma suala la elimu.
Shule nyingi mpya za sekondari za kata zilifunguliwa mwaka jana na mwaka huu zimekuwa zikikabiliwa na matatizo ya madawati, majengo ya utawala, nyumba za walimu pamoja na walimu wa kufundisha ambapo hali hiyo imesababisha wazazi kupewa mzigo mzito wa michango.
Hata hivyo, taarifa zilizopatikana zinaeleza kuwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, imeagiza wanafunzi wote waliofukuzwa warudi shuleni hata kama hawajatoa michango hiyo.