KAIMU Katibu wa Taasisi ya Amina Chifupa, Hassan Chifupa, amewaomba wale wote wenye mapenzi mema na marehemu Amina wasaidie kuchangia mfuko huo ili ukamilishe majukumu yake.
Akizungumza na waandishi wa habari jana kwenye Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Dar es Salaam, Chifupa alisema lengo la taasisi hiyo ni kuenzi yale yote marehemu Amina aliyokuwa akiyafanya kwa masilahi ya taifa.
Akifafanua, alisema baadhi ya mambo aliyokuwa akiyafanya ni kupiga vita mihadarati, kuendeleza michezo, kutoa misaada kwa watoto wanaoishi katika maisha magumu na mengineyo mengi.
Mzee Hamisi Chifupa, baba mzaza wa marehemu Amina Chifupa, aliyekuwa mbunge wa Viti Maalum (CCM), aliwasihi wabunge na madiwani waliofanya kazi na marehemu, nao kuchangia taasisi hiyo kama ishara ya kumuenzi marehemu.
Alisema michango hiyo itapokelewa kutumia akaunti ya taasisi hiyo Na. 01J1014153400 iliyopo Benki ya CRDB au fedha taslimu italipiwa katika ofisi yake iliyopo jengo la Uchumi Project, Barabara ya Shekilango karibu na Chuo cha Ustawi wa Jamii.