LICHA ya serikali kupitia Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), kupiga marufuku uuzwaji wa vipodozi vyenye kemikali, dawa hizo zinaendelea kuuzwa kwa wingi jijini hapa.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima, umebaini kuwa, vipodozi hivyo vinaingizwa kwa njia ya magendo kutoka nchi jirani kisha kusambazwa kwa wafanyabiashara wa maduka na kuuzwa kwa siri.
Kwa majuma kadhaa sasa, gazeti hili limebahatika kuwaona wafanyabiashara wakubwa na wadogo wakiingiza na kuuza vipodozi hivyo haramu.
Aidha, uchunguzi huo umegundua kwamba, wafanyabiashara hao wanafanya shughuli hizo kwa kubadili makasha ya vifaa vyenyewe na kuweka dukani, kwa lengo la kuficha muonekano wa makasha ya vifaa hivyo.
Mbali na kubadili makasha, njia nyingine inayotumiwa na wafanyabiashara hao katika kuficha vipodozi hivyo ni kuviweka kwenye maboksi yaliyochakaa.
Kutokana na kutapakaa kwa vifaa hivyo, imebainika pia kuwepo kwa baadhi ya viongozi na watendaji wa serikali wanaoshirikiana na wafanyabiashara hao katika kusafirisha na kuuza vipodozi hivyo.
Maeneo yaliyokithiri vipodozi hivyo ni Makoroboi, Mabatini, Kirumba, Igoma na Mtaa wa Uhuru.
Baada ya TFDA kupiga marufuku uingizwaji na uuzwaji wa vipodozi hivyo, mamlaka hiyo inafanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maduka na kuwakamata wafanyabiashara wa vipodozi hatarishi na haramu.