WANARIADHA wawili wa timu ya taifa ya Tanzania jana waliondoka nchini kwenda China, kushiriki mbio za Standard Chartered Marathon, zinazotarajiwa kutimua vumbi Jumapili nchini humo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Katibu Msaidizi wa Chama cha Riadha Tanzania (RT), Julius Musomi, alisema kuwa chama chake kimewateua wanariadha hao wawili - Paul Sumaye na Fabiola William - ili kuiwakilisha nchi katika mbio hizo.
Musomi alisema kuwa walipata mwaliko wa kushiriki katika mashindano hayo kutoka benki hiyo, ambao ndiyo wadhamini wakuu wa mashindano hayo yanayoshirikisha mataifa mbalimbali duniani.
Naye Meneja Uhusiano wa benki hiyo, Joanitha Mramba, akizungumza katika hafla ya kuwakabidhi bendera ya taifa wanariadha hao, aliwatakia kila la heri na kuwa wanaamini wataipeperusha vema bendera ya Tanzania na kurejea na ushindi.
Mramba alisema kuwa mbali na kuwatakia mafanikio wachezaji hao, pia benki yake imetoa vifaa mbalimbali watakavyotumia wanariadha hao na gharama mbalimbali za mashindano hayo.
Alivitaja baadhi ya vifaa hivyo kuwa ni tiketi za kwenda na kurudi kwa wachezaji, suti za michezo, fulana, kofia, gharama za chakula, malazi na mahitaji mengine yatakayojitokeza katika mashindano hayo.