WAFANYAKAZI 12 wa Chama Cha Wafanyakazi wa Vyuo Vikuu, Elimu ya Juu, Utafiti na Wafanyakazi Waendeshaji (RAAWU), tawi la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), wamefungua kesi ya madai katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, dhidi ya katibu mkuu wao wa taifa.
Wafanyakazi hao wanaowakilishwa na Chistmas Swai, wanatetewa na wakili Dk. Sengondo Mvungi.
Wanaiomba mahakama iwaruhusu kufungua shauri la kufuta maamuzi ya Kamati ya Utendaji wa Taifa ya Raawu ya kuwachukulia hatua za kinidhamu viongozi wa tawi lao, kwa kusimamisha malipo ya ada za uanachama yasipelekwe taifa.
Kwa mujibu wa hati ya madai hayo, tawi la Raawu chuoni hapo lilisimamisha kupelekwa makao makuu makato ya ada za uanachama za kila mwezi kutokana na uongozi wa makao makuu kushindwa kutekeleza wajibu wao wa kutetea maslahi ya wanachama.
Wanachama hao wanalalamikia mishahara midogo na kushindwa kwa uongozi wa taifa kufanya mazungumzo na serikali kupandisha mishahara ya wafanyakazi wa chuo.
“Uongozi chuoni hapo ulifanya juhudi za kuwasiliana na viongozi wa serikali na kufanya majadiliano hayo, hivyo hawaoni kazi wanayofanya viongozi wa taifa hadi kustahili kupelekewa makato ya ada za wanachama.
Wanachama hao 12 waliopeleka hati ya maombi ya kuruhusiwa kufungua shauri la kufuta maamuzi ya uongozi wa taifa, wanapinga uamuzi wa uongozi wa taifa kuwasiliana moja kwa moja na mwajiri wao, ili kufanya mazungumzo ya kulipwa na mwajiriwa moja kwa moja badala ya kupitia akaunti ya tawi.
Wafanyakazi katika vyuo vikuu vingine kama vile Chuo Kikuu cha Afya cha Muhimbili wamekwishaanza mchakato wa kujiunga na wafanyakazi wa tawi la UDSM, jambo linaloashiria kushindwa kwa uongozi wa Raawu Taifa kukidhi matakwa ya wafanyakazi.