MADHARA ya ujenzi wa hoteli za kitalii katika Hifadhi ya Taifa Serengeti bila kufanya tathimini ya uharibifu wa mazingira, yameanza kuonekana kutokana na wananchi wa Mugumu Mjini kutishia kuishitaki halmashauri hiyo, baada ya hoteli hizo kutupa taka mjini hapo.
Uamuzi wa wananchi hao wa Mtaa wa Sedeco mjini kutaka kuiburuza halmashauri mahakamani, unatokana na kukithiri kwa taka katikati ya makazi ya wananchi, zinazosababishwa na hoteli ya kitalii ya Serena, huku uongozi wa halmashauri hiyo ukiwa kimya.
Akizungumza na Tanzania Daima, mkazi wa mtaa huo Issa Marare, alisema wanataka kuchukua uamuzi huo kutokana na malalamiko yao kwa uongozi wa halmashauri kutofanyiwa kazi.
Alisema wanaathirika na taka hizo kutokana na harufu mbaya, na pia watoto wao hucheza kwenye dampo hilo wakiokota chupa na taka mbalimbali zikiwemo kondomu.
“Tumefikia uamuzi wa kutaka kuishitaki halmashauri kutokana na kutuona sisi kama sehemu ya taka, huku wataalam wa afya wakiwa kimya, hali ambayo inatupa shaka kuwa kuna utaratibu wa maelewano baina ya wamiliki wa hoteli na wao,” alisema.
Diwani wa Kata ya Mjini, Ryoba Charles, alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kuwa alilikuta mwaka 2005.
Alisema amekuwa akilizungumza suala hilo katika vikao vya Baraza la Madiwani.
Alisema Hoteli ya Serena baada ya kuona wananchi wamecharuka, wamekuwa wakimwaga taka hizo usiku.
Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya, Dk. Maungo Kawa, naye alikiri kupokea malalamiko hayo na kusema suala hilo liko kwa mkurugenzi kwa kuwa zinahitajika fedha za kuhamisha dampo hilo.
Hoteli nyingi zilizomo ndani ya hifadhi zinadaiwa kutokuwa na maneo ya kutupa taka, hivyo kulazimika kuzitupa katika makazi ya watu.