SERIKALI imeipa notisi kampuni ya kushughulikia makontena katika Bandari ya Dar es Salaam, ikiitaka wakae pamoja na kujadili mkataba baina yake na kampuni hiyo.
Hayo yalibainishwa bungeni jana na Waziri wa Miundombinu, Andrew Chenge, wakati akitoa majibu ya ziada kwa swali la nyongeza lililoulizwa na Mbunge wa Same Mashariki, Anna Malecela (CCM).
Mbunge huyo aliuliza kwanini
serikali iiamuru PSRC kukubali kurefusha mkataba baina ya serikali na TICTS? Alisema kuwa walipotembelea PSRC wakati akiwa mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu, ofisa mmoja wa mamlaka hiyo aliwaeleza kuwa agizo la kurefusha mkataba huo lilitoka ngazi za juu serikalini.
Chenge alisema serikali ililazimika kurefusha mkataba huo kabla muda wake wa awali haujamalizika kutokana na mazingira ya uwekezaji mkubwa ambao mwekezaji alipaswa kuufanya katika mradi huo.
Alisema mkataba wa awali ulikuwa wa miaka 10 na isingewezekana kwa mwekezaji kufanya uwekezaji mkubwa na kurudisha fedha zake katika kipindi hicho.
Hata hivyo, Chenge alisema kutokana na masuala yaliyojitokeza, serikali imelazimika kumwandikia mwekezaji huyo, kumuomba waujadili upya mkataba huo.
Alisema kwa bahati nzuri, mwekezaji huyo ameonyesha nia ya kukubaliana na notisi hiyo na hivyo mazungumzo hayo yatafanyika kwa lengo la kuweka mazingira yatakayozinufaisha pande zote.
Akijibu swali la msingi lililoulizwa na Mbunge wa Singida Kusini, Mohammed Misanga (CCM), Naibu Waziri, Dk. Milton Mahanga alisema tangu 2000 hadi 2007, TICTS ilikuwa imenunua vifaa kadhaa vya kufanyia kazi ya kupakua, kupakia, kupanga, kuhamisha na kuhifadhi makontena.
Aidha, alisema serikali imeona umuhimu wa kuiwezesha Mamlaka ya Bandari (TPA) kuanzisha kitengo cha makontena, ili kupanua huduma hiyo na kuiboresha bandari ya Dar es Salaam.
Katika kutekeleza azma hiyo, Dk. Mahanga alisema TPA tayari imeshanunua eneo lenye ukubwa wa hekari 19.6 sehemu ya Kurasini kwa ajili ya upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam.