TIMU ya Coastal Union ya jijini hapa, imewafungia wachezaji wanne kwa kipindi cha miezi sita, huku ikimsimamisha kwa muda usiojulikana kipa wake namba moja, Ismail Suma, aliyewahi kuidakia Yanga.
Wengine waliofungiwa kwa miezi sita, ni Sadaat Salim, Thabit Msulwa, Amani Kimbede na Leon Kimathi kwa kile kilichoelezwa kuwa utovu wa nidhamu walioonyesha wakati timu hiyo ikiwa kambini mkoani Morogoro.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Coastal Union, Salim Bawazir, adhabu kwa wachezaji hao imetolewa jana na Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo, iliyokutana kujadili masuala kadhaa ya timu hiyo ikiwamo mwenendo wake katika raundi ya pili ya Ligi Kuu.
Akifafanua, Bawazir alisema wakiwa kambini Morogoro, wachezaji hao waligoma kushiriki katika mazoezi ya mchana katika kujiandaa na mechi dhidi ya Polisi Dodoma na walipoulizwa na kocha wa timu hiyo, walitoa lugha chafu dhidi yake na viongozi wa timu.
“Nakumbuka baada ya kumaliza mechi yetu na Polisi Moro, ilibidi tuendelee na mazoezi kama kawaida, lakini cha ajabu, wachezaji hawa walimgomea kocha na baadhi ya viongozi waliokuwepo huko bila sababu za msingi, hali hii haiwezi kuvumilika,” alisema.
Hata hivyo, kuna habari kuwa kusimamishwa kwa kipa Suma, ni baada ya kutuhumiwa kuwa aliihujumu timu hiyo siku ilipocheza na Yanga Februari 2, ambako Coastal Union ilifungwa 4-0, ingawa viongozi wa timu hiyo, wamesema wanaendelea na uchunguzi.
Bawazir, alisema licha ya timu hiyo kufanya vibaya katika mechi nne za mzunguko wa pili wa ligi inayoendelea, inatarajia kufanya vizuri katika mechi yake ya leo dhidi ya timu ya Prisons ya Mbeya itakayopigwa Uwanja wa Mkwakwani jijini hapa.
Mechi nyingine ya ligi hiyo leo itakuwa katika Uwanja wa Jamhuri kwa Polisi Morogoro kukipiga na Manyema FC.