HABARI MPYA KITAIFA DAR MIKOANI TAHARIRI MAKALA MICHEZO
jumapili, 21 septemba 2008
Pekua Tovuti
Gazeti la Jana
Matangazo
Bei zetu
Wasiliana nasi
Tuma habari


Mkeo anapotaka simu ya pili wakati ada ya mtoto mgogoro!
 
Tom Kilumbi


NI dhahiri Watanzania wengi tunafahamu umuhimu wa kuwa na simu za mkononi katika dhana nzima ya kurahisisha mawasiliano miongoni mwetu, hali ambayo kwa namna moja au nyingine inaharakisha pia maendeleo yetu kijamii.

Pamoja na kutambua hilo, lakini si Watanzania wote wenye simu za mikononi wanaofahamu vema matumizi ya simu zao au lengo kamili la mtu kumiliki simu kama lilivyokusudiwa na watengenezaji wake.

Wapo ambao simu kwao ni kama mapambo na wengine ni kwa ajili ya kujionyesha (showing off) kuwa wanazo, hata kama uwezo hauruhusu kufanya hivyo!

Kama vilivyo vitu vingine vya elekroniki kuwa na matoleo mbalimbali kila baada ya kipindi fulani kupita, hivyo hivyo ndivyo ilivyo kwa simu za mkononi pia. Hivyo, kwa wale wenye nafasi zao, si ajabu kuwaona wakimiliki kila aina ya toleo la simu linaloingia sokoni kama vile wale wapenda kwenda na fasheni za mavazi wafanyavyo katika kutimiza azma yao ya kuvaa kulingana na mavazi yaliyopo sokoni kwa kipindi hicho.

Ni dhahiri kwa wale wenye uwezo wao kifedha si kitu cha ajabu kumiliki matoleo tofauti ya simu kila yaingiapo sokoni kwa kuwa hilo haliwezi kuharibu utaratibu wa maisha yao kiuchumi. Lakini kwa wale wenzangu na mimi, hata kama na wao wanapenda kuwa na matoleo mapya ya simu, ila si jambo la busara kukimbilia kununua hizo simu wakati kuna mambo mengine muhimu katika familia zao yanayotakiwa kufanyiwa kazi yakiwa bado hayajakamilishwa kwa wakati huo.

Mtu tayari anayo simu ambayo inamwezesha kufanya mawasiliano kamili na watu wengine wote anaotaka kuwasiliana nao, lakini kwa sababu tu kuna toleo jipya la simu lipo mtaani ambalo lina vikorombwezo kibao vya ziada, basi na yeye anaamua kukimbilia kuinunua hiyo simu mpya kwa bei mbaya. Wakati inapowadia muda wa kulipa ada ya shule ya watoto wake inakuwa ni mgogoro mtupu!

Anahangaika kwenda huku na huko kutafuta wapi kwa kukopa, ili angalau watoto waweze kuendelea na masomo kana kwamba wakati anakimbilia kununua hiyo simu eti ili aende na wakati, hakujua kuwa kuna kulipa ada ya shule ya watoto wake!

Kama nilivyotangulia kusema kuwa, kama uwezo unaruhusu kukununua kila toleo la simu liingialo mtaani si vibaya, nasema tena si vibaya pia kuwa na simu zaidi ya moja, hata kama una simu tano na kuendelea, ili mradi una uwezo wa kuzimiliki, kuzitumia na kuzihudumia bila ya kuathiri mambo mengine katika taratibu zako za maisha ya kila siku pamoja na familia yako. Hilo kwa kifupi halina tatizo, lakini siyo umiliki wako wa simu ugeuke kuwa mzigo katika maisha yako na jamii inayokuzunguka. Hilo kwa kweli halikubaliki.

Nimelazimika kusema haya kutokana na jamaa zangu fulani kujikuta katika migogoro na wake zao ambao kwa hivi sasa baadhi yao wana simu ‘mbili mbili’ na wengine nao wakiwa katika harakati za kubanana na waume zao, ili wawanunulie simu nyingine, ili na wao wawe nazo mbili mbili.

Kumnunulia mkeo simu hata kama ni ya pili, ya tatu au zaidi ya hapo si vibaya, lakini angalau kuwe na sababu za msingi za kufanya hivyo. Si tu kwa sababu fulani na fulani wanazo, basi na yeye anataka kuwa nayo. Hilo kwa kweli ni sawa na ufujaji wa vyanzo vya pesa ndani ya familia.

Kama bibiye ana biashara au ajira ambayo kwa namna moja au nyingine unaweza kusema kuwa inahitaji awe na simu zaidi ya moja, ni bora katika kuweka mambo sawa kiutendaji basi itafutwe simu nyingine ya pili. Angalau hilo lina nafasi yake na linakubalika bila kipingamizi chochote. Lakini pale bibiye anapodai simu nyingine zaidi kwa nguvu zote wakati hana shughuli yoyote ile kiutendaji inayohitaji kuwa na mawasiliano zaidi ya kutumia simu moja, kwa kweli hilo si jambo la busara hata kidogo.

Vile vile ni vema kutambua kuwa pindi unaponunua simu nyingine ina maana umeongeza matumizi pia kwa ajili ya kununulia muda wa maongezi. Sasa hizo gharama zote za nini za kumiliki simu mbili wakati huna shughuli yoyote ile inayokuingizia kipato zaidi ya kumsubiri mumeo mwenye simu moja akuachie pesa ya matumizi ya nyumbani na wewe unazichikichia pesa hizo hizo za matumizi kwa kuongezea vocha katika simu zako!

Asilimia kubwa ya muda wako unautumia kwa kuwepo nyumbani au saluni, sasa simu mbili za nini? Hayo siyo mambo kabisa ya kuendekezwa katika dunia hii ya leo.

E-mail: tkilumbi@yahoo.com


juu

Warning: mysql_connect() [function.mysql-connect]: Can't connect to local MySQL server through socket '/var/run/mysqld/mysqld.sock' (2) in /hermes/bosweb/web098/b983/glo.freemanm2/include/comment.php on line 9
I cannot connect to the database because: Can't connect to local MySQL server through socket '/var/run/mysqld/mysqld.sock' (2)