WACHIMBAJI wadogo wa madini ya tanzanite, maarufu kama Wana-apolo, Mererani wilayani Simanjiro, Manyara, wamelaani kitendo cha Wizara ya Nishati na Madini kuwahukumu kwa kuwafungia migodi yao hata kabla uchunguzi wa madai ya ulipukaji wa mabomu katika migodi hiyo haujakamilika.
Wakati wachimbaji wadogo wakifungiwa uchimbaji, wenzao wa Kampuni ya TanzaniteOne wanaendelea kuchimba.
Kufungiwa kwa migodi hiyo ya wachimbaji wadogo, kumeelezwa ni hatari kwani zaidi ya Wana-apolo 1,000 hawana kazi za kufanya, hali iliyodaiwa inaweza kusababisha vurugu na upotevu wa amani baada ya kukosa masurufu ya kujikimu kimaisha.
“Migodi ya wachimbaji wadogo imefungwa, sawa, lakini kwanini ifungwe hiyo tu, wakati madai ya ulipukaji wa bomu yalitokea katika migodi ya wachimbaji wakubwa na hakuna hata mitobozano inayoonyesha kuwa wachimbaji wadogo walipenya na kwenda kulipua mabomu hayo?” alihojia mmoja wa Wana-apolo ambaye hakutaka kutajwa jina.
Baadhi ya wataalamu wa machimbo hayo wamedai hali hiyo inaweza kusababisha tafrani na kwamba zipo taarifa zisizothibitishwa zinazodai Wana-apolo hao wanaweza kuvamia sehemu za biashara ndogo ndogo katika machimbo, kwani tayari kina mama lishe wameanza kulia baada ya kudhulumiwa vyakula na wachimbaji hao.
Migodi 17 ya wachimbaji wadogo ilifungiwa wiki iliyopita kwa kile kilichoelezwa hadi uchunguzi ufanyike jambo linalopigiwa kelele na wachimbaji hao.