SERIKALI imeombwa kuchukua hatua za haraka za kulinusuru Shirika la Reli Mkoa wa Tanga ambako ofisi yake imefungwa na watumishi wote kuondolewa kazini kwa zaidi ya miezi miwili baada ya shirika hilo kubinafsishwa.
Ombi hilo lilitolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mohamed Abdulaziz, wakati wa mazungumzo ya pamoja kati ya madiwani, watendaji wakuu wa halmashauri ya mji huo na Waziri Mkuu, Edward Lowassa.
Mkuu huyo, alimtahadharisha Waziri Mkuu kuwa iwapo jitihada za haraka hazitafanyika, baada ya muda mfupi upo uwezekano wa baadhi ya vyuma vya reli za mkoa huu kufunguliwa na wahalifu kisha kuuzwa kama chuma chakavu.
Alisema, jambo hilo litachangia kwa kiasi kikubwa kurudisha nyuma maendeleo ya mkoa na serikali kupata hasara na akamweleza Waziri Mkuu kwamba, tegemeo la watumishi wa reli ni kuboreshewa miundombinu na hali za maisha yao baada ya kuingia mwekezaji jambo ambalo ni kinyume na matarajio.
“Waziri Mkuu, tegemeo langu lilikuwa kwamba baada ya shirika hilo kubinafsishwa mwekezaji, basi angelenga katika kuboresha huduma mbalimbali za miundombinu ya kiutendaji.
“…Pia tulitegemea ongezeko la safari za treni za mizigo kutoka bandarini, badala yake ameamua kufunga ofisi na kuwaondoa watumishi wote mpaka walinzi, inasikitisha. Jambo hili litaathiri mapato yetu na kuporomosha uchumi wa Mkoa wa Tanga,” alifafanua Abdulaziz.
Alibainisha kuwa, ofisi yake imeiandikia Wizara ya Miundombinu barua kuhusu tatizo hilo na kuliwasilisha kikaoni hapo ili Lowassa, aliunge mkono na kutafuta njia mbadala ya kulinusuru shirika hilo.
Mkuu huyo alisema, azma ya serikali kuu ni kuona serikali za mitaa zinajiendeleza kwa lengo la kuwarahisishia wananchi upatikanaji wa huduma bora.
“Wanafahamu kwamba serikali imedhamiria kuboresha maisha yao na hali ya usafirishaji wa njia ya reli kwa kujenga bandari ya Tanga, katika eneo la Mwambani na ujenzi wa barabara ya Tanga-Horohoro… lakini naomba niseme kwamba haya yote yatafanikiwa iwapo tu na reli yetu itafanya kazi,” alisisitiza.