WAKAZI wa Jiji la Mbeya, wameelezea tabia ya kutokuwa makini katika uchaguzi wa madiwani wenye uwezo, kuwa ndiko kunakokwamisha mipango mingi ya maendeleo ya jiji hilo.
Hali hiyo inatokana na taarifa mbalimbali za mapato na matumuzi ya fedha za serikali zilizopokelewa kwenye halmashauri ya jiji hilo kushindwa kusimamiwa vizuri, hivyo kujikuta ikipatiwa hati chafu ya matumizi.
Baadhi ya wakazi wa jiji hilo waliozungumza na Tanzania Daima, waliwalaumu madiwani wa halmashauri hiyo kuwa hawaonyeshi umakini katika kutetea maslahi ya wananchi kiasi cha kuwafikisha wananchi kukosa huduma muhimu.
Wananchi kadhaa waliohudhuria kikao maalumu cha baraza la madiwani wa jiji hilo walisema kuwa kitendo cha halmashauri hiyo kupewa hati chafu ya mahesabu na kusababisha inyimwe ruzuku ya sh milioni 440.8 ni cha aibu.
“Tatizo madiwami wetu wengi tumewachagua bila kupima uwezo wao wa kuchanganua mambo na kujua majukumu yao ndani ya halmashauri, huku wakiwaona watendaji wanaoharibu na kuwafumbia macho, waige sehemu nyingine,” alisema mkazi mmoja wa Uyole.
Alisema kuwa tangu Mkuu wa Mkoa, John Mwakipesile aingie madarakani, amekuwa haridhishwi na taarifa za mapato na matumizi ya jiji hilo, hali ambayo imekwenda sambamba na taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.
Mkazi wa eneo la Soweto aliyejitambulisha kwa jina moja la Mama Light, alisema huduma nyingine kama taa za barabarani zilipaswa kuwepo kwenye mji huo, lakini unasongwa na giza zito huku madiwani wakishuhudia.
Alisema katika kipindi cha miaka miwili sasa, shughuli za maendeleo zinaonekana kusimama huku barabara na miundombinu mingine ikionekana kuchakaa kwa kasi, hali ambayo inatia shaka matumaini ya jiji hilo kufikia malengo yake.
“Lazima madiwani wetu wabadilike, hii ni aibu kubwa kwa jiji, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na serikali yake, kwani kitendo cha kunyima ruzuku kilipaswa kuwawajibisha watendaji na si kuwasukumia uzembe huo wananchi wasiojua lolote au tulikosa kuchagua,” alisema mwananchi huyo.
Alisema inashangaza kuona madiwani hao wakimwandama vikali Mstahiki Meya ya jiji hilo, Athanas Kapunga huku wakijua wazi kuwa wanayo sauti kubwa na kura ya veto dhidi ya mtendaji yeyote wa jiji hilo anayeonekana kwenda kinyume na maadili ya utumishi.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Assumpta Ndimbo alinukuliwa katika baraza hilo akilaumu wingi wa madiwani waliopo, lakini hawasaidii kulifanya jiji hilo lipatiwe hati safi, ili kusaidia kusukuma maendeleo ya wananchi.
“Hati chafu inawaondolea sifa na heshima katika nafasi zenu na hali hii haionyeshi kuwepo kwa kasi mpya katika utendaji wenu wa kazi ndani ya halmashauri hii,” alisema Ndimbo.
Kutokana na kukwama mambo kadhaa katika jiji hilo, inadaiwa kuwa mambo si shwari kiasi cha kufikia madiwani kadhaa kusakamana kwa vitisho na kauli kali, huku wakielekeza mashambulizi yao kwenye kamati za siasa za CCM kuomba msaada.
Jiji la Mbeya linaongozwa na idadi kubwa ya madiwani kutoka CCM na ndio wanaotuhumiana kutokuwa makini na usimamizi wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo ile ya ujenzi wa shule za sekondari na huduma nyingine za kijamii kuendelea kukwama.