MRADI wa Taasisi ya Maendeleo ya TechnoServe unatarajia kupokea msaada wa dola milioni 46.9 (zaidi ya sh milioni 50) kutoka kwa Mfuko wa Maendeleo wa Bill & Melinda Gates kwa ajili ya kuendeleza zao la kahawa kwa wakulima wa nchi za Afrika Mashariki ikiwamo Tanzania.
Meneja mradi huo kwa upande wa Tanzania, Adolph Kumburu, alisema zaidi ya wakulima 180,000 wadogo wadogo wa kahawa katika nchi za Afrika Mashariki ikiwamo Tanzania, hasa Mkoa wa Arusha watanufaika na msaada huo.
“Ongezeko na mahitaji ya kahawa duniani litawawezesha wakulima wadogo wadogo kujipatia kipato kikubwa mara tu watakapoboresha ubora wa kilimo cha zao hilo.
“Maelfu ya wakulima ambao kwa zaidi ya miaka mitano tumekuwa tukijishugulisha nao kwa njia mbalimbali wameweza kwa kiasi kikubwa kujipatia kipato kikubwa.
“Kuongezeka kwa kipato cha wakulima hao kumekuwa na maendeleo katika familia zao, mambo ambayo yamewawezesha pia kuanza kuwasomesha watoto wao katika shule zinazotoa elimu bora,” alisema Adolph.
Msaada huo wa maendeleo wa mfuko Bill & Melinda Gates ulitangazwa hivi karibuni na Mwenyekiti mshiriki wake, mfanyabiashara Bill Gates katika kongamo la maendeleo ya uchumi duniani linalofanyika nchini Uswisi ikiwa ni hatua yake ya kwanza katika kuisaidia sekta ya maendeleo ya kilimo.
Katika hatua hiyo, mfuko huo uliozinduliwa katikati ya mwaka 2006 unatarajia kutoa dola milioni 360 katika maendeleo ya kilimo.