na Chris Mang’era, Tarime
MFUNGWA katika gereza la Wilaya ya Tarime, Charles Mtuki Werema (35), amefariki dunia baada ya kunaswa na umeme.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mara, David Saibullu, aliwaambia waandishi wa habari kuwa tukio hilo lilitokea juzi, saa tano asubuhi, wakati mfungwa huyo, mkazi wa Kijiji cha Mbalibali, wilayani Serengeti, akikata mti umbali wa takriban mita 300 kutoka gerezani hapo.
Saibullu alisema mfungwa huyo alipanda juu ya mti mkubwa ulioko nyuma ya jengo la zamani la Halmashauri ya Wilaya ya Tarime na kuanza kukata matawi ya mti huo kwa ajili ya kuni za kutumia gerezani.
Katika harakati hizo, alikata tawi likaangukia nyaya za umeme zilizoko jirani na mti huo mbichi na kuzifanya zigusane ndipo akashika tawi hilo na kujaribu kulinasua kutoka kwenye nyaya hizo.
Kwa mujibu wa Kamanda Saibullu, kabla ya kulinasua tawi hilo, mfungwa huyo alipigwa shoti akaanguka chini na kuzimia, ndipo alipokimbizwa katika Hospitali ya Wilaya ya Tarime ambako alifariki dunia muda mfupi baadaye.
Hata hivyo, juhudi za kumpata Mkuu wa Gereza la Tarime, ili kujua mfungwa huyo alikuwa akitumikia kifungo cha muda gani na kwa kosa gani ziligonga ukuta baada ya mwandishi kumpigia simu ya mkononi mara kadhaa bila mafanikio.
Wakati huo huo, mkazi wa Mtaa wa Saronge, mjini Tarime, John Waisiko (35), alivamiwa na majambazi wakamjeruhi kwa kupigwa risasi mguu wa kushoto na kumkata panga usoni.
Kamanda Saibullu alisema tukio hilo lilitokea saa 3:30 usiku wa kuamkia jana, wakati Waisiko akisubiri kufunguliwa lango kuu la nyumbani kwake akitokea katika biashara yake ya mgahawa.
Alisema majambazi hao walifanikiwa kutoroka baada ya kumjeruhi na kumpora Waisiko sh 120,000 alizokuwa nazo mfukoni.