HABARI kubwa katika gazeti hili, toleo la leo, inahusu mauaji ya kinyama ya Tumaini Mbaga, aliyekuwa dereva wa Naibu Waziri wa Usalama wa Raia, Mohamed Aboud.
Katika habari hiyo, Jeshi la Polisi limeeleza kuwa mwili wa dereva huyo ulikutwa kwenye pori la Kwembe Kipera, katika mpaka wa Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani, ukiwa umetenganishwa na kichwa.
Awali, ilielezwa dereva huyo kutoweka na gari hilo Januari 19 mwaka huu, lakini gari hilo lilipatikana siku saba baadaye likiwa kwenye maegesho ya magari eneo la CCM Tabata Kimanga.
Kutoweka kwa gari hilo na dereva wake kuliacha maswali mengi kutokana na mazingira yaliyokuwapo kabla na baada ya kubainika kutoweka kwao.
Mauaji haya yaliyofanywa ni ya kinyama, kwani kumchinja mtu ni zaidi ya uharamia, ni unyama wa hali ya juu. Ni jambo lisilovumilika hata kidogo kwa binadamu mwenye akili timamu.
Tunaamini kuwa, kuchinjwa kwa dereva huyo kunatokana ama na visasi kati ya waliofanya unyama na marehemu au hasira za kushindwa kutoweka na gari hilo kwa namna yoyote ile.
Vitendo hivi vya kinyama havifai kuwepo kwenye jamii yetu hasa tukizingatia kuwa misingi ya taifa hili ni amani na utulivu, ambavyo tunahitaji kuvienzi.
Mauaji hayo si tu yanasikitisha na kuogofya, bali yanaiacha yatima familia ya marehemu huyo, hivyo ni jukumu la serikali kuwapa uangalizi mzuri watoto na mke wa marehemu Mbaga.
Hali hii inatishia usalama wa madereva wengine wa viongozi na raia wema. Inasikitisha kuona tunaishi na binadamu wenye roho za kinyama kiasi cha kumchinja mwenzie kama kuku, tena bila huruma.
Tunakemea kitendo hicho na kulitaka Jeshi la Polisi kuhakikisha watuhumiwa wa mauaji haya wanatiwa mbaroni na hatua za kisheria zaidi kuchukuliwa dhidi yao.
Lakini kwa upande mwingine, tunalihusisha tukio hilo na genge la wahalifu wa magari ambalo kwa muda mrefu sasa limekuwa likisumbua ukanda wa Afrika, hasa kusini mwa Jangwa la Sahara.
Aidha, tunaishauri serikali kutenga maeneo maalumu yenye usalama wa kutosha kwa ajili ya kuegesha magari ya viongozi wake.
Hii inatokana na ukweli kwamba magari hayo ya gharama kubwa yanayonunuliwa kwa kodi zetu yapo kwenye hatari ya kuibwa zaidi kutokana na ufinyu wa maegesho. Hii ni aibu kwa serikali.
Ni wazi kwamba watu waliofanya kitendo hicho wafahamu fika kuwa magari ya serikali yakiwamo ya mawaziri hayana usimamizi maalumu wa kuyalaza, hivyo kufanikisha wizi huo kirahisi.
Hata hivyo, tukio hili linatufanya tujiulize, kwa nini magari ya serikali yalazwe kwenye ofisi za CCM ambazo hazina ulinzi madhubuti hadi kuyalaza mitaani?
Tukumbuke kuwa mwaka jana, serikali kupitia Wizara ya Miundombinu ilitangaza zabuni ya kutafuta kampuni itakayoweka mitambo maalumu ya kufuatilia mienendo ya magari yote ya serikali ili kuyalinda kutokana na madai ya kuwapo kwa matumizi mabaya na kuzuia wizi.
Hivi mpango huo uliishia wapi au ndiyo yale yale ya kuahidi na kusubiri mpaka madhara kama haya yatokee ndipo serikali ikurupuke?
Tunaamini kama serikali ingeweza kuwa na mtambo wa kuweza kufuatilia mienendo ya magari yake, ni wazi kwamba gari hilo la Naibu Waziri lingeibiwa na wala kifo cha kutisha cha dereva huyo kisingetokea.
Kutokana na tukio hili, serikali sasa inapaswa kuweka utaratibu mzuri wa kudhibiti magari yake kwa kuyalaza katika ofisi zake, ili kuzuia wizi pamoja na hujuma nyingine.
Pia tukio hili linaikumbusha serikali kwamba vitendo vya uhalifu, vikiwamo vya wizi wa magari, bado vinaendelea, na kwamba zinatakiwa juhudi nyingine za kuvunja uti wa mgongo wa uhalifu nchini.