HABARI kubwa katika gazeti hili leo inahusu kauli ya Katibu wa Uenezi na Itikadi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), John Chiligati, kwamba hoja ya ubadhirifu wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), iliyoibuliwa bungeni na Dk. Willbrod Slaa haikuasisiwa na upinzani.
Katika habari hiyo, Chiligati anasema kuwa wakati Dk. Slaa ambaye ni Mbunge wa Karatu (CHADEMA), alipokuwa akiitoa bungeni mwaka jana, tayari serikali ilishaanza kuishughulikia.
Aidha, katibu huyo wa CCM alikwenda mbali zaidi na kusema, serikali ilichelewa kuifanyia kazi kwa miezi mitatu kutokana na mchakato wa kumtafuta mkaguzi wa nje, hali iliyosababisha wapinzani kuidakia kabla ya uchunguzi kukamilika.
Kauli hiyo inakuja baada ya Rais Jakaya Kikwete, kutengua uteuzi wa aliyekuwa Gavana wa BoT, Dk. Daudi Ballali, na wananchi kumtaka kuchukua hatua zaidi huku wakimpongeza Dk. Slaa kwa ujasiri wa kuitoa hoja hiyo hadharani.
Tunamshangaa Chiligati, CCM na serikali yake kwa kukataa hata ukweli ulio wazi kuhusu suala hili. Sababu ya kufanya hivyo ni pale hoja hii ilipotolewa bungeni kwa mara ya kwanza.
Tunakumbuka namna ambavyo viongozi wa serikali bungeni walivyohaha kutaka kuizima hoja hiyo huku Spika Samuel Sitta, akisema wazi kwamba ushahidi wa kwenye mtandao hautoshi kumtuhumu mtu.
Wakati Dk. Slaa akitoa hoja hiyo, baadhi ya mawaziri na viongozi wa juu wa CCM walisema kauli za wapinzani kuhusu ufisadi huo ni uchochezi na kupakana matope kunakofanywa na kambi ya upande wa pili.
Pamoja na mawaziri hao, Rais Kikwete alikaririwa akisema kuwa kelele za wapinzani kuhusu ufisadi hazimnyimi usingizi lakini hakuwahi hata siku moja kusema kuwa ni hoja ya chama chake.
Sote tu mashahidi kuwa bila ujasiri wa Dk. Slaa kuiondoa hoja yake na kuamua kuiwasilisha kwa wananchi, hakuna kitu ambacho kingefanyika kutokana na ukweli kwamba baadhi ya watuhumiwa wa ufisadi huo ni viongozi wa serikali.
Kuibuka kwa Chiligati na kusema wazi kuwa hoja ya ufisadi ni yao, tunaona hiyo ni propaganda za CCM kwa sababu ya uchaguzi mdogo wa ubunge kule Kiteto mkoani Manyara.
Katika hili ni lazima serikali na CCM wakubali kuwa wanajaribu kubadili kibao kwa lengo la kujisafisha machoni pa wananchi kwa kujifanya kuwa wao ndio waanzilishi wa hoja ya ufisadi wa BoT.
Tunasikitishwa na kauli hii ya kiongozi wa juu wa CCM ambaye kwa namna moja au nyingine tunadhani kwamba anaanza kujenga hoja ya uwezo wa chama chake katika uchaguzi huo mdogo ambao unaweza ukatoa matokeo yenye taswira ya vikao viwili vya Bunge vilivyopita.
Yawezekana majigambo ya CCM yakawa sawa, lakini tunabaki njia panda kwamba kama kweli hoja ile ilikuwa ni ya chama hicho tawala, ilikuwa inasubiri nini?
CCM ndiyo yenye dhamana ya taasisi zote, kuanzia wizara na vitengo vyake, kwa kuwa imeshika dola. Ikiwa viongozi wake waligundua kuwepo kwa ufisadi na wakaamua kukaa kimya huku Chiligati akisema walikuwa wanachunguza, hatuelewi walichokuwa wakikichunguza.
Isitoshe, kama hoja ilikuwa ni ya CCM, ilikuwaje chama hicho tawala kilitaka kuizima? Kwa hili, tunaona kwamba CCM imepora hoja, lakini tunasikitika kusema kwamba imekumbuka kujifunika shuka wakati kumekucha. CCM imechelewa, hoja ya ufisadi wa BoT ilianzishwa na Dk. Slaa.