MSANII nguli wa maigizo nchini, Fatma K. Makame ‘Joanita’ ameanzisha kundi lake binafsi la sanaa hiyo, linalokwenda kwa jina la ‘Hamadombe Art Group’.
Akizungumza na Tanzania Daima jijini Dar es Salaam jana, Joanita alisema kuwa makao makuu ya kundi hilo linalokusanya wasanii wengi chipukizi ni Mwananyamala jijini Dar es Salaam.
“Nimeanzisha kundi hilo tangu Machi mwaka huu, ambako lengo langu kuu ni kutoa fursa ya ajira kwa ndugu zangu wenye vipaji vya uigizaji, pamoja na vijana wengine,” alisema Joanita.
Aidha, alisema kuwa tayari wameishatoa filamu moja inayokwenda kwa jina la ‘Sonia’ ambako baadhi ya wasanii katika filamu hiyo ni wadogo zake wawili, Fatma Makame na Nasra Mohammed.
Kadhalika, alisema kuwa hivi sasa wako katika maandalizi ya mwisho ya filamu zao mbili ambazo ni ‘Mjomba Feki’ pamoja na ‘Urithi wa Kifo’.