TIMU kumi za soka za Tanzania Bara, zinatarajiwa kushiriki michuano ya vijana chini ya miaka 20 ya Rollingstone, ambayo mwaka huu itafanyika Makamba nchini Burundi kuanzia Julai 7.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Rollingstone, Issa Karata, timu 24 zitashiriki mashindano hayo na zimepangwa katika makundi sita, ambapo timu nyingine zinatokea Burundi, Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), Uganda na Zanzibar.
Alizitaja timu za Tanzania zilizoingia katika mashindano hayo kuwa ni Azam FC, Bishop High School, Chakyi Academy, Coastal Union, Rollingstone, Ruvu Shooting, Simba, TAYFA Academy, Yanga na Young Life.
Alisema, timu zote zinatakiwa kwenda na vyeti halisi vya kuzaliwa vya wachezaji wake, ili kuthibitisha umri wao na Kamati ya Mashindano itakuwa na uamuzi wa mwisho kuhusu umri wa mchezaji yeyote.
“Kila timu inatakiwa kuwa na wachezaji 20 na viongozi watano, ambao watagharamiwa na waandaaji kwa huduma za malazi na chakula kwa muda wote wa mashindano hayo yaliyoanzishwa miaka 13 iliyopita,” alisema Karata.